Karibu Katika mtandao wa Shirika la Cartoon Forum Tanzania, katika mtandao huu utapata kujua mambo mengi kuhusiana na Shirika hili pia kupata matukio, picha na katuni mbalimbali zenye kuelimisha. Hivyo ni nafasi yako kujifunza na pia kutoa maoni yako, KARIBU SANA...

Monday, December 11, 2017




Washiriki wa Mkutano wa kupiga vita Rushwa
ya ngono wakionesha mabango yenye ujumbe wa vita hiyo.









Rushwa ya ngono sehemu za kazi huondoa heshima ya utu, hupunguza tija.

Na Adam Malinda,
Kwa Hisani ya Cartoon Forum Tanzania.


RUSHWA ya ngono ni aina mojawapo ya rushwa ambazo zimeleta athari kubwa katika  Jamii hasa katika maeneo ya kazi, baadhi wameshindwa kuichukia kwa kutokujua, wengine kwa kutofahamu namna inavyodhalilisha utu wa mtu, lakini baadhi yao kwa kutofahamu namna ya kupambana na changamoto inayowakabili ambayo ni kujiamini na kusimamia kile wanachokiamini. 
Tunapozungunzia rushwa ya ngono sehemu za kazi maana yake imeleta unyanyasaji, ukatili na kunyimwa haki ya mfanyakazi mwenyewe, pale anapostahili mwanamke kupandishwa cheo, kuongezewa mshahara, kulipwa malupulupu stahiki, kuendelea kazini, kuepuka kupunguzwa na masuala mengineyo kama hayo.

Mwanamke ni muathirika namba moja wa rushwa ya ngono kwa sababu ya historia ya mfumo dume uliojengeka miongo na karne kadhaa zilizopita, ambapo Mwanamke amechukuliwa kama chombo cha kumtumikia Mwanaume.

Kilio na masikitiko makubwa katika ofisi za umma na binafsi ni Wanaume kuwa na mamlaka za juu na kuwaweka baadhi ya wanawake kama makatibu mukhtasi, wanaoongoza idara za chini, jambo ambalo baadhi ya wanawake walinyanyaswa kijinsia kwa kutoa rushwa za ngono kwa masharti ili wabaki kazini.


Tatizo kubwa ambalo limechangia hali hiyo ni usiri wa kitendo hicho na mbinu zinazotumika kumfikisha mahali pagumu Mwanamke kiasi cha kuamua, “amtumikie kafiri apate mradi wake “.

Wapo baadhi  ya wanaume nao wamekumbana na rushwa za ngono kwa mazingira ambayo walishawishiwa kufanya mapenzi ili waweze kitimiza matakwa yao ya kimaisha, lakini rushwa hii pia imekuwa ngumu kuthibitika ambapo pia malalamiko ya namna hiyo wanaume wameyachukulia ni aibu kuliko ilivyo kwa wanawake.

Jukumu lililopo kwa sasa wanajamii wajenge  hisia za utambuzi kwa kuichukia rushwa hii, kujitambua thamani ya uhuru wa mawazo, utu, na maamuzi makini, kwani kufikiri kwa njia rahisi, hutatua matatizo kwa njia ya mkato, kukata tamaa, husababisha kuingia katika mitego ya rushwa za ngono ambazo hupoteza haki ya msingi na utu wa mtu.

Jamii ilichukulie suala la rushwa ya ngono kama chukizo linalobeba dhambi kama zilivyo rushwa nyingine kwa kuwa madhara yake ni makubwa, kwa mfano unapoanzisha mahusiano  sehemu ya kazi, uwajibikaji hupungua, upendo na mtazamo miongoni mwa mashirikiano na wafanyakazi wenzako hupungua, kuanza kufanya kazi kwa majungu badala ya umahili, lakini pia huwapunguzia ari wafanyakazi wenzako, mkuu wa kazi hupoteza heshma anayostahili kuwa nayo, lakini pia ni udhalilishwaji mkubwa hasa kwa mwanamke aliyekubali kurubuniwa na kujikuta ameangukia katika mtego wa rushwa ya ngono. Kwa hakika jamii nzima inapaswa kusema Hapana kwa rushwa ya ngono ili kurudisha utu wa mwanamke sehemu za kazi.


Mwisho.

No comments:

Post a Comment